Ads 468x60px

Thursday 5 March 2015

UFAHAMU UYOGA WA ASILI KUTOKA TANZANIA NA FAIDA ZAKE.



Uyoga ni zao la viumbe hai viitwavyo kuvu (fungi). Tanzania inao utajiri mkubwa wa uyoga wa asili. Uyoga wetu wa asili hupatikana wakati wa msimu wa mvua tu. Hili ni tatizo kubwa kwa vile wananchi walio wengi hupenda kula uyoga wakati wote.

Kwa sababu ya upatikanaji wa uyoga kwa msimu, na kwa vile aina nyingine za uyoga wa kienyeji zina sumu, tumefanya jitihada za kuanzisha kilimo cha uyoga ili kukidhi mahitaji ya wananchi kwa mwaka mzima. Pamoja na kutoa lishe bora kwa watu, uyoga pia unaweza kuzalishwa kama zao la biashara.

UMUHIMU WA ZAO LA UYOGA.


Uyoga kama chakula una viinilishe vingi vilivyo muhimu kwa afya ya binadamu. Uyoga una protini kati ya 3-4. Pia una vitamini B, C, D na K. Uyoga pia una madini yanayohitajika katika mwili wa binadamu.

Uyoga ukitumika kama sehemu ya chakula cha familia mara kwa mara hutibu au kuzuia magonjwa kama vile saratani, vidonda vya tumbo, shinikizo la damu pia huongeza kinga ya mwili.

Kilimo cha uyoga huchangia pato la kaya na hutoa ajira. Kilimo hiki ni kizuri kwa wazee, akina mama na vijana kwa vile hakihitaji mtaji mkubwa kuanzisha na mavuno hupatikana baada ya muda mfupi. Aidha kilimo hiki hakihitaji eneo kubwa kama mawazo mengine kwani uyoga huoteshwa ndani ya banda.

MAHITAJI YA KUANZISHA KILIMO CHA UYOGA.

1. Mbegu

Kama mazao mengine; ili kuanzisha kilimo cha uyoga unahitaji mbegu. Maabara za mbegu za uyoga ziko Uyole hutoa aina mbalimbali za uyoga kwa bei ya nafuu.

2. Masalia ya mazao ya kilimo.

Kilimo cha uyoga hutumia masalia ya mazao ya kilimo kwa mfano majani ya mpunga, maharage, migomba, magunzi, mabua na ngano. Kwa ujumla kilimo cha uyoga hutunza mazingira kwa vile uchomaji wa masalia ya mazao ya kilimo huharibu mazingira.

Mabaki ya kilimo uyoga yanaweza kutumika kama mbolea, chakula cha mifugo au kuzalisha nishati ya gesi.

3. Banda.

Uyoga hulimwa ndani ya banda. Banda ligawanywe katika vyumba viwili, chumba chenye giza na chumba chenye mwanga na hewa. Banda liezekwe kwa nyasi (bati huleta tofauti ya joto kati ya mchana na usiku).

4. Kichanja au meza.

Kwa ajili ya kupozea majani na vifaa vya kupandia uyoga.

5. Pipa au sufuria kubwa.

Kwa ajili ya kuchemsha ili kuua wadudu na vimelea vya magonjwa kwenye masalia ya mazao ya kilimo.

6. Mifuko ya plastiki na kamba.

Uyoga hupandwa kwenye mifuko ya plastiki ambayo baada ya kupandwa hufungwa kwa kamba.

7. Hatua za kilimo cha uyoga.

- Fanya usafi kwenye banda la kulimia uyoga.
- Chambua masalia ya mazao ya kilimo (ondoa yenye rangi ya kijani) kisha osha kuondoa vumbi na uchafu mwingine.
- Weka maji theluthi moja ya chombo cha kufukizia.
- Jaza vimeng'enywa kwenye pipa, funika na fukiza angalau kwa saa mbili (tangu mvuke unavyotokea juu ya mfuniko).
- Ipua kwenye kichanja au meza iliyooshwa.
- Ikisha poa , angalia unyevu uliobaki kwenye vimeng'enywa kwa kukamua vimeng'enywa. Kama matone ya maji yanatoka; anza kupanda. Kama maji yanachuruzika bado kwa hiyo endelea kusambaza ili maji yatoke.
- Baada ya kunawa, sia kwenye mfuko wa plastiki tabaka ya vimeng'enywa ikifuatiwa na mbegu mpaka mfuko umejaa. Mwishoni weka tabaka la mbegu kisha funga mfuko kwa kamba.
- Toboa mashimo kama 8 kupitisha hewa juu, katikati na chini ya mfuko; kwa kutumia uma au kijiko.
- Weka mifuko kwenye chumba chenye giza ili mbegu ziote na utandu ufunike mfuko wote . Hii itachukua wiki 2-3 kutegemea na hali ya hewa.
- Hamisha mifuko kwenye chumba chenye mwanga na hewa ili uyoga uote.
- Uyoga utaota baada ya siku 7 mpaka 10. Vuna baada ya siku 4. Endelea kuvuna mpaka mavuno yatakapofifia (baada ya miezi miwili hivi).

Imeandaliwa Buberwa Robert

5 comments:

Anonymous said...

Shukrani.
Je ni Kweli kwamba Kuna aina za Uyoga ( eg. oyster mushroom) haziitaji chumba cha giza?

Anonymous said...

Kwetu Bukoba ni walaji sana wa hili zao tatizo ni Lile lile-zao msimu na hawalifanyi la biashara...hii ni fursa,thanks Robert

FREBU SPORTS said...

Ni kweli uyoga wa aina hii ya Oyster hazihitaji chumba cha giza ndugu

FREBU SPORTS said...

Ni kweli uyoga wa aina hii ya Oyster hazihitaji chumba cha giza ndugu

FREBU SPORTS said...

Asante sana mdau kutoka Bukoba nimefurahi sana kujumuika nawe hapa. Endelea kupitia blog hii upate mengi zaidi. Nasi twakutegemea kwa mengi zaidi